Friday, October 27, 2017

Bocco.....Wachezaji Simba Waomba Acheze

WACHEZAJI wa Simba kwa pamoja wamelazimika kumfuata kocha wao Joseph Omog na kumsihi ampange kikosi cha kwanza John Bocco katika mchezo wa leo dhidi ya Yanga.


Yanga inakairibisha Simba kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam katika mchezo namba 58 wa Ligi Kuu Bara ukiwa ni wa kwanza kwao kwa Dar es Salaam msimu huu wa ligi.

Mmoja wa wachezaji wa Simba, aliliambia Championi Jumamosi kuwa, ilibidi wamfuate kocha wao na kumuomba ampe nafasi Bocco katika kikosi cha kwanza kwani ni mpambanaji anayewaweza Yanga.

“Tumemuomba kocha ampe nafasi Bocco kwani anaweza kupambana na mabeki wa Yanga kama Yondani (Kelvin), unajua wanacheza kibabe sana sasa ukimuweka mtu mwingine hatawaweza.

“Bocco hata akichezewa rafu huwa hakati tamaa, yeye anaenda tu na mabeki watatumia muda mwingi kumzuia yeye huku sisi wengine tukiweka sawa mipango ya ushindi.

“Kocha ametusikiliza lakini hatujui kama uamuzi wake huo atautekeleza au vinginevyo lakini naamini Bocco akicheza tutakuwa na nafasi kubwa ya kushinda mechi hii,” alisema mchezaji huyo.

Bocco aliyejiunga na Simba akitokea Azam FC, alikuwepo kambini Zanzibar na Simba licha ya kusumbuliwa na jeraha la kifundo cha mguu. Kama Omog raia wa Cameroon atamuanzisha Bocco, Simba katika safu yake ya ushambuliaji itakuwa na Emmanuel Okwi na Bocco huku pembeni wakicheza Shiza Kichuya na Haruna Niyonzima.

No comments:

Post a Comment